Saturday, 14 June 2014

HILI NDIO JENGO REFU KULIKO YOTE MJINI IRINGA



Hili ndio jengo refu kuliko yote mjini Iringa. Kwa miaka mingi jengo hili limekuwa halitumiki kwa kazi zake zilizokusudiwa. Jengo hili lina kinu kikubwa cha kusaga na kuhifadhi nafaka. Awali lilikuwa likimilikiwa na Shirika la Usagishaji la Taifa (NMC). 

MAPEMA mwaka jana serikali iliamua kukikabidhi kinu hicho cha NMC Iringa kwa Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko.
 

Kinu hicho chenye kiwanda cha kusaga unga, kina vienge virefu vyenye uwezo wa kuhifadhi tani 13,500 za nafaka, na maghala mawili yenye uwezo wa kuhifadhi tani 3,500 za nafaka na tani 1,100 ya unga.
 

Makabidhiano ya kinu hicho yanayohusisha pia majengo na mali zake nyingine yalifanyika April 10, 2011 katika hafla fupi iliyohudhuriwa na uongozi wa mkoa wa Iringa, bodi hiyo, wafanyakazi wa NMC na wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula.
 

Kinu hicho ambacho kwa muda mrefu kimekuwa hakitumiki kwa kazi zake zilizokusudiwa kilikamilika ujenzi wake mwaka 1975 uliofanywa kwa ushirikiano kati ya serikali ya Jamuhuri ya Muungano ya Tanzania na shirika la Kimataifa la Misaada la Sweden (SIDA).
 

Kilifunguliwa rasmi kwa ajili ya kuanza uzalishaji Julai 6, 1976 na aliyekuwa Rais wa Msumbuji Marehemu Samora Machel.


Pamoja na kinu hicho kukabidhiwa kwa bodi hiyo, matarajio ya wakazi wengi wa mkoa wa Iringa kwamba kingeanza kufanya kazi na kusaidia harakati za serikali za kuongeza ajira mpya kupitia sekta hiyo ya kilimo, zinazidi kufifia.


Kimsingi ni kwamba hakuna kinachoendelea katika kinu hicho zaidi ya majengo yake mengine kupangishwa kwa wafanyabiashara mbalimbali.
 

Wafanyabishara hao wanaendelea na shughuli zao katika majengo ya kinu hicho pamoja na Mwakilishi wa shirika la Consolidated Holding Corporation (CHC) lililochukua nafasi ya shirika la Kurekebisha Mashirika ya Umma, Joseph Mapunda kuahidi kwamba wangepewa notisi baada ya makabidhiano hayo.
 

Wapangaji walio katika majengo ya kinu hicho ni pamoja na wakala wa kampuni ya Bia Tanzania (TBL), wakala wa safari za anga, Bar maarufu ya Dragon na ofisi za wadau mbalimbali.

Like Page Yetu Hapa Kuungana Nasi Facebook

0 comments:

Post a Comment